Taarifa za kuchukiza na kutisha kuwa kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)
mbunge wa Shinyanga Mjini na Waziri mdogo (Nishati na Madini) Steven Masele
pamoja na wenzake, walipanga na kuratibu mpango mchafu wa kuwaua Katibu
mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk Wilbroad Slaa
na Mkurungenzi wa Mawasiliano na Uhusiano, mbunge wa Ubungo, John Mnyika zinaiweka CCM pabaya. Je Masele ni nani? Je yuko peke yake katika ugaidi huu
unaoonekana kupangwa na watu wengi zaidi yake? Je atachukuliwa hatua au
kufumbiwa macho kama mwenzake, Mbunge wa Iramba na Waziri mdogo wa Fedha, Mwigulu Nchemba, aliyetuhumiwa kwa vitendo vya kigaidi akapandishwa cheo?
Je imeishia wapi kesi ya kubambikizwa ya mkurugenzi wa usalama wa CHADEMA,
Wilfred Rwakatare? Si wameuia kimya kimya baada ya mbinu zao za kigaidi
kufichuliwa? Je watanzania wataendelea kujiruhusu kutawaliwa na chama
kilichoishiwa kiasi cha kujigeuza kundi la kigaidi? Je njama kama hii ingeelekezwa
kwa Katibu mkuu wa CCM Abdulrahaman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi,
Nape Nnauye serikali ingeendelea kujifanya hamnazo wala haijui kitu? Mbona
tunatumia sheria kihuni na kibaguzi hivi?
Diwani wa kata ya Ngokolo mjini Shinyanga, Sebastian Peter alifichua kuwa
waliahidiwa mamilioni ya fedha kutekeleza mauaji ya wawili tajwa walipokuwa
Shinyanga kikazi mwezi Februari. Peter alikaririwa akisema, “Baada ya maongezi
ya aina mbali mbali na Mchange tulishindwa kupata muafaka lakini tuliendelea
kuwasiliana na aliporudi Shinyanga akatueleza kuwa kuna mpango mzuri wa fedha
na kwamba utasimamiwa na Waziri Masele na kwamba tutapata sh. milioni 180
kila mmoja.” Hivi kweli kuna ushahidi zaidi ya huu kupaswa kumfungulia mashtaka
Masele na wenzake? Kama huu ni uzushi mbona mtuhumiwa haendi mahakamani kusafisha jina lake? Peter anaendelea, “Mkakati huo ulianza kuratibiwa na Mwenyekiti wa
UVCCM, Abbakari Gulam ambaye ni mtoto wa Meya wa Shinyanga, wakiwa na
Habib Mchange, kisha tuliona mkakati unatekelezwa na mbunge wa Shinyanga
mjini, Stephen Masele, Nape Nauye, Januari Makamba, Mwigulu Nchemba na
Ridhiwani Kikwete.”
Kwanza, ni aibu kwa mbunge, anayepaswa kuwa mfano wa jamii, kugeuka
gaidi. Pia ni aibu kwa serikali kutochukua hatua stahiki. Kitendo cha Masele
kushiriki ugaidi na uvunjaji wa sheria licha ya kumuaibisha kama mwakilishi wa
wananchi, kinawaibisha na kuwadhalilisha wale waliomwamini uwakilishi. Pia,
kwa nafasi yake, Masele alipaswa abanwe aachie ngazi kwa vile ameaibisha kazi ya
ubunge na bunge kwa ujumla. Mbunge anayeweza kupanga kutekeleza ugaidi
hapaswi kuendelea kuwa bungeni wala uraiani bali gerezani akingojea kesi yake
kusikilizwa na kutolewa hukumu. Kunajengeka dhana kuwa Masele alitumwa na
wenye serikali inayomilki taasisi na vyombo vyote, hatachukuliwa hatua. Ndiyo
maana mamlaka hazimchukulii hatua. Je kweli Tanzania inafaa kuendelea
kutawaliwa na chama na serikali na watu wanaoweza kudiriki kutenda ugaidi
halafu wakaendelea kulindana?
Pili, kwa wanaojua uhusiano baina ya Masele na mtoto wa kigogo mkubwa
wa CCM ambaye pia ni kigogo wa serikali, hawashangazwi na hisia kuwa
anatumiwa tu na mtandao mkubwa. Wengi wanajua kuwa, pamoja na udhaifu
wake kitaaluma, Masele aliteuliwa kwenye nafasi aliyo nayo kutokana na ukaribu
wake na mtoto wa kigogo huyu ambaye ana ushawishi mkubwa katika masuala
mengi yanayohusiana na mamlaka ya baba yake. Pia kwa wanaojua makundi ya
kigaidi yanavyofanya kazi, Masele hawezi kuwa peke yake. Lazima kuna watu
wakubwa na makundi makubwa yaliyomtuma kupanga njama hizi. Huenda ndiyo
maana akapigiwa kampeni na kuteuliwa uwaziri wakati hana sifa. Walimuopoa
mapema wakijua wanavyoweza kumtumia wakati ukitimu.
Tatu, siasa za kichovu, kikatili na kuishiwa sera tulizoea kuzisikia na
kuzishuhudia kwa majirani zetu hasa Kenya ambapo chama tawala cha wakati ule
kiliwaua makada wake wengi kiliodhania walikuwa tishio kwa ulaji wa bwana
mkubwa. Pia, tulizoea kusikia watoto wa watawala wa huko nao wakijigeuza
watawala tusijue yatafika hata kwetu. Je imekuwaje tumefika hapa? Bila shaka,
ni matokeo ya ufisadi na siasa za kifisi ambapo kila mwenye kupata madaraka
huyatumia vibaya kuibia umma na kujitajirisha kiasi cha wasaka tonge kuwa tayari
kuua watu wasio na hatia ilmradi wapate madaraka ambayo ni hati ya kuibia umma
kwao. Hivyo, si ajabu kushuhudia magaidi, majambazi hata wauza mihadarati
wakijitokeza kutumia fedha zao zitokanazo na jinai yao kusaka nafasi za kisiasa na kuendeleza jinai yao bila kuguswa wala kuzuiliwa hata kama ni kwa kuua wenzao.
Nne, wahanga wa mpango huu mchafu na CHADEMA wanapaswa kuomba
vyombo vya kimataifa vinavyoshughulikia ugaidi kuingilia kati kwa sababu
mamlaka za Tanzania haziwezi kufanya hivyo kutokana na kutekwa na CCM.
Tano, watanzania wajulishwe kupitia mikutano mbali mbali aina ya utawala
unaoanza kujengeka chini ya CCM ambayo imeamua, kwa tamaa ya madaraka,
kujigeuza kuwa kundi la kigaidi. Chama kilichofikia kiwango hiki hakipaswi
kuendelea kuvumiliwa kuwa madarakani. Kuna haja ya kuwahakikisha taasisi za
kimataifa zinazoshughulikia ugaidi zinajulishwa angalau zitoe maelekezo hata
maoni yake.
Sita, walengwa wasijue yamekwisha. Wanapaswa kuchukua hatua madhubuti
na tahadhari vya hali ya juu kwa vile kilichowasukuma CCM kutaka kuwaua bado
kipo pale hasa ikizingatiwa kuwa CHADEMA ndiyo tishio lao. CCM iko tayari
kufanya lolote liwe haramu au halali kuhakikisha inabakia madarakani ikifanya
ufisadi na ugaidi wake kama kawaida. Hili halivumiliki. Upinzani unapaswa
kulichukulia tishio hili kwa uzito unaostahili.
Saba, kwa upande wake, licha ya kushinikiza Masele na genge lake la kigaidi
lishitakiwe, kuna haja ya kumbana rais kuhakikisha anamwajibisha ili iwe rahisi kumshughulikia kisheria.
Tumalizie kwa kulaani mchezo huu mchafu ambao kama hautazuiliwa kwa
nguvu ya umma unaweza kulitumbikiza taifa kwenye machafuko na mauaji ambayo yangeweza kuzuilika. Wakati wa kuzuia zahama hii ni sasa.
Chanzo: Tanzania Daima Agosti 27, 2014.
UMESIKIA KUHUSU NJAMA ZA KUMUUA SILAA: NI ZAIDI YA MASELE
Reviewed by habari motto
on
3:37 PM
Rating: