Naibu Waziri Wa Elimu Afafanua Utaratibu Wa Kupata Cheti Mbadala

NAIBU Waziri wa Elimu ,Sayansi na Teknolojia,William OleNasha,amefafanua utaratibu wa kupata cheti mbadala/uthibitisho kwa mtu aliyepoteza cheti ambapo ameeleza kuwa Baraza la Mitihani litafanya kazi hiyo kwa muda usiozidi siku 30.

Ole Nasha aliyasema hayo jana bungeni mjini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Mafinga Mjini,Cosato Chumi (CCM) lililokuwa likihoji ‘’Je ni utaratibu gani unaotumika pale mtu anapopoteza cheti ili aweze kupata cheti kingine’’?,Je ni unapata cheti halisi au nakala? na ni taratibu gani anatakiwa kuzifuata  mtu ili ombi lake lifanyiwe kazi ipasavyo na bila kucheleweshwa?.

Katika majibu yake Naibu Waziri huyo alieleza kuwa mhitimu aliyepoteza cheti hupatiwa cheti mbadala/uthibitisho wa matokeo kwa kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kuhusu upotevu wa cheti na kupata hati ya upotevu.

Pia  mtu aliyepotelewa na cheti atatakiwa kutangaza gazetini kuhusu upotevu huo  kwa lengo la kuutaarifu umma ili kusaidia kukipata na endapo cheti hakitapatikana hata baada ya kufuata utaratibu huo ,mhitimu atajaza fomu ya ombi la cheti mbadala /uthibitisho wa matokeo na kuiwakilisha Baraza la Mitihani.

‘’Baada ya mhitimu kujaza fomu hiyo Baraza la Mitihani hufanya uchunguzi wa uhalali wa umiliki wa cheti husika na kutoa huduma stahiki ,wahitimu waliofanya mtihani kuanzia Mwaka 2008 ambao vyeti vyao vina picha hupatiwa vyeti mbadala ‘’alisema na kuongeza kuwa

“Na waliofanya mtihani kabla ya Mwaka 2008 hupatiwa uthibitisho wa matokeo ambao hutumwa kwa waajiri wao au mahali pengine kwa mahitaji yaliyotolewa na mwombaji na kundi hilo halipewi cheti mbadala’’

Alisema cheti mbadala kinachotolewa ni cheti halisi ambacho huongezwa maandishi yanayosomeka ’DUBLICATE’ kuonyesha kuwa cheti hicho kimetolewa mara ya pili.
Naibu Waziri Wa Elimu Afafanua Utaratibu Wa Kupata Cheti Mbadala Naibu Waziri Wa Elimu Afafanua Utaratibu Wa Kupata Cheti Mbadala Reviewed by habari motto on 9:50 AM Rating: 5
ads 728x90 B
Powered by Blogger.